TAIZÉ

Bruda Roger na upatanisho wa Wakristu

 

Makala hii imeandikwa na Mgr Gerard Daucourt, Askofu wa Nanterre, kwenye gazeti la “La Croix”, siku ya Jumatano tarehe 16 Agosti 2006.

“Mkuu huyu wa Taizé alijazwa na hamu ya upatanisho ambayo iligusa vilindi vya nafsi yake na kumhimiza kutafuta njia za upatanisho.

Tarehe 16 Agosti 2005, ilikuwa siku ambayo Taizé ilichomwa moyo; wakati bruda Roger alipokuwa katika sala na mabruda wake pamoja na maelfu ya vijana, alishambuliwa katika kanisa ambalo jina lake limebeba wito wa Taizé: kanisa la upatanisho.

“Katika ujana wangu” anaandika Bruda Roger, “nilishangazwa sana kuona jinsi Wakristu – ambao kimsingi wanaishi kwa ajili ya Mungu mwenye upendo - wakitumia nguvu nyingi kuhalalisha utengano wao. Kwa hiyo nikajiambia, ni muhimu kujenga jumuiya kusudi watu watafute kuelewana na kupatana siku zote, na kupitia njia hii kutengeneza fumbo la umoja” Kilichofutata kinafahamika sana: wakivutiwa na urahisi wa sala na maisha ya jumuiya, na kuguswa na matumaini ya mabruda, makumi elfu ya vijana huja Taizé kila mwaka, kuuliza maswali yao, kutoa vilio vyao vya mahangaiko, kushirikishana matumaini yao, kugundua kuwa Kristu anawapenda, kujifunza kuishi katika umoja wa kanisa na kuwa waletaji wa amani.

Kwa hiyo hii jumuiya pamoja na vijana, wanatafuta kudhihirisha mapatano ambayo Kristu anatuitia, kati ya wakristu na wanadamu wote. Mabruda pia wana habari na midahalo migumu ya kiteolojia au mikutano – rasmi na yenye umuhimu – kati ya viongozi wa makanisa, lakini wao kwanza hutoa habari njema kwa vijana pamoja na namna ya kuzipokea.

Bruda Roger alijazwa na hamu ya upatanisho ambayo iligusa vilindi vya nafsi yake na kumhimiza kufungua njia za upatanisho. Kwa unyenyekevu alishirikishana hali na msukumo huu aliojisikia “nimeweza kujifahamu kama mkristo kwa kujipatanisha imani yangu pamoja na fumbo la imani ya kikatoliki, bila kuvunja umoja na mtu yeyote” baadhi ya wanateolojia waliikosoa, wengine walisema Bruda Roger hakuwa mteolojia. Baadhi ya viongozi wa kanisa walilazimisha utambulisho rasmi wa usemi huu utakaoeleweka zaidi.

Bruda Roger aliupenda mwili wote wa Kristu na alikiri hili katika maisha yake yote. Bila ya kuikana asili yake, wala kumpinga mtu yeyote, alitamani kupatanisha ndani yake yale yote ambayo Mungu ametoa katika makanisa ambayo bado yametengana. Akigundua umuhimu wa huduma ya papa ya umoja ulimwenguni, aliishika imani ya Ekaristi na huduma ya kanisa katoliki pia muda huo huo aliishi katika utajiri ambao Mungu ameuzawadia makanisa ya Kiorthodoksi na Kiprotestanti. Bila ya wasiwasi wala mateso, aliuishi kabisa upatanisho wa makanisa. Je haitoshi kutambua bila kuhukumu na kusema kwamba kile tulicho nacho hapa ni pekee, na kutotafuta sababu za kuonesha kuwa haiwezekani?

Je tunakubali kuruhusu angalau tuulizwe? Je tunakubali angalau kuwa na wasiwasi endapo huu ”upekee” siku moja hautapungua, ili ufungue njia kwa watu wengi? Kumsikiliza Bruda Roger, tunaweza kujikumbusha kwamba utengano wetu unagongana na mapenzi ya Kristo, na kwamba ekumeni ni kubadilishana zawadi, ya kwamba tunahitajiana, pia upatanisho sio kuishi kwa amani katika utengano, ila ni matumani, kutajirishana pamoja na kushirikiana. Labda baadaye tutajua namna kuyasaidia makanisa yetu yapunguze kuliko sasa kushikwa katika kurudi katika utambulisho wao. Ninaongea binafsi, kwa sababu mabruda wa Taizé hawajawahi kutamani kutoa masomo kwa mtu yeyote na pia kuwa ”mabingwa wa kiroho”, hata wa ekumeni. Wakati Yohani Paulo wa pili alipowatembelea owaka 1986 alisema kwamba wito wa jumuiya yao ni ”kwa namna fulani, ni wa kuendelea”. Katika kitabu chake kizuri kuhusu Taizé, Profesa Olivier Clement aliongea kuhusu ”hali ya msingi unaoendelea”.

Kifo cha kikatili cha Bruda Roger mwaka mmoja uliopita, katika moyo wa wito wa Taizé, ni sehemu ya huu ’“mpambamoto wa kuendelea”. Kupitia sauti ya mkuu wao mpya, mabruda wa Taizé wanatuambia kuwa hawajioni kama wahusika pekee katika mpambamoto huu. (“sisi ni watu masikini ambao tunahitaji umoja wa Kristu ili kuendelea mbele katika imani”). Bruda Alois pamoja na mabruda wake wanaendelea mbele katika njia iliyowekwa na Brother Roger. Tayari wanaishi kile cha kanisa ambacho kinaonekana ni kimoja na wanawaongoza vijana kuelekea katika vyanzo vya imani pamoja.

Ilirekebishwa mara ya mwisho: 27 September 2007